
Enyi wakenya wapenda amani niliposema hamna viongozi mlinifokea sana na kukinga kabila zenu zaidi hata ya dini yake Mwenyezi Mungu.
Niliposema tunatawaliwa na waongo mlinidharau na kunitusi kwasababu waongo hao ni wa kabila lenu.
Uhuru Kenyatta amewatia wakenya hofu, ameonyesha wazi kuwa hana doa la uongozi iwapo atatukimbilia sisi ambao serikali hiyo hiyo yake imetupora, kutuponda na kutufukarisha zaidi.
Serikali hiyo hiyo yake ikatuibia katika zile sakata za Eurobond na Nys. Serikali hiyo hiyo ikawapiga watoto wetu na gesi ya kuwatoa machozi kwa kupinga unyakuzi wa ardhi yao ya shule.
Uhuru Kenyatta anatucheka, Uhuru Kenyatta anatuchezea shere kwa kutuuliza jambo ambalo yeye mwenyewe ana suluhu juu yake.
Uhuru Kenyatta alichaguliwa kama Rais na wala sio Chifu wa kijiji anayesubiri amri kutoka kwa wakuu wake. Uhuru Kenyatta anafaa kila akilala na kuamka kukumbuka kuwa yeye ndiye Rais na kutuuliza sisi afanye nini ni kutudharau kama waliomchagua.
Wiki iliyopita ilikuwa wiki ya vihoja kutoka kwa Rais Uhuru Kenyatta. Oktoba ishirini ilikuwa ni Siku ya kuadhimisha babake Uhuru Kenyatta.
Siku iliyogeuzwa jina na kupewa jina la siku ya mashujaa kwani sifa hizo zilistahili mashujaa wote wa Kenya waliopigana na wakoloni kukomboa Kenya na wakenya kwa jumla.
Tangu jina hilo la Kenyatta Day kuondolewa na kuwa Mashujaa baadhi ya watu waliotengwa na waliochangia pakubwa katika kupigania uhuru wa taifa hili walianza kujiskia kuwa miongoni mwa wakenya walioheshimika kutokana na mchango wao.
Huku wakenya wakiendelea kujivinjari siku hiyo Uhuru Kenyatta baada ya kutuuliza afanye nini aliwataja mashujaa aliopendelea na kuwasahau wengine labda kutokana na chuki za kisiasa.
Jameni, huwezi futa au bomoa historia ya taifa hili hata kwa nyundo. Kwa kuwataja mashujaa wachache na kuwaacha wengine imeonyesha hali halisia yako kama kiongozi.
Wakenya sasa wamejua wewe ni mtu aina gani. Naomba kwa moyo mkunjufu nikukumbushe majina ya mashujaa jabali uliokataa kuwataja.
JARAMOGI OGINGA ODINGA
Huyu ni jabali. Simba wa mapinduzi na kiboko cha waingereza. Kama hukumbuki jina lake yeye ndiye aliyekuwa apewe Urais wa taifa lakini akakataa kwa kusema kuwa hadi babako mzazi Jomo Kenyatta aachiliwe kutoka gereza ndipo Kenya itajipatia uhuru wake.
Tafadhali soma kitabu cha NOT YET UHURU na kama huna naomba nikununulie licha ya hali ngumu ya maisha ninayopitia na ninayo amini inasababishwa na serikali yako.
Jina la Jaramogi litasalia katika vitabu vya historia vibaraka wapende wasipende.
Jaramogi ndiye aliyetufikisha hapa tulipo kutokana na mateso aliyopitia kutufanya sisi sote huru kutoka serikali ya Hayati mzee Jomo Kenyatta na Daniel Toroitich Arap Moi.
KENETH STANLEY NJINDO MATIBA
Rais wa watu miaka ya nyuma. Kiboko cha demokrasia na kiongozi wa upinzani enzi zake. Matiba si jina la kaimati ila ni jina lililo na heshima ya hali ya juu.
Licha ya kufungwa jela na kuteswa, Matiba na mashujaa wengine walihakikisha kuwa tumepata vyama vingi vya kisiasa na kuwakomboa wakenya kutoka kwa wakoloni weusi walioiba kwa niaba ya waliopigania uhuru wa taifa hili.
Leo hii Matiba anaishi kama sungura huku akipoteza kila kitu alichokuwa nacho. Subirini afe mtudanga’nye alivyokuwa mtu mashuhuri na wa maana.
Leo hii ni mgonjwa na hata hamna soni wala sura ya kumsaidia.
RAILA AMOLLO ODINGA.
Hili jina likitajwa wakabila wote wakuu hujificha. Huyu ni jabali aliyefungwa gereza kwa miaka mingi akipigania haki ya wakenya. Bado yeye amesalia kuwa Baba ya wakenya na kipenzi cha wote.
Wanaomchukia hawana sababu ila chuki za kikabila.
Wengine wanamchukia tu kwa sababu walizaliwa wakiambiwa na wazazi wao eti yeye ni mtu mbaya. Wengine hata hawana mali lakini wanaambiwa Raila atawanyanga’nya mali zao.
Kenya ya sasa maskini anadangany’wa na semi za longo longo eti atafurushwa na hali hana hata nyumba ya mbwa wala yake aliyoijenga ya kujisitiri.
Mashujaa wengine ni: PIO GAMA PINTO, MAKHAN SINGH, TOM MBOYA, JM KARIUKI, NGUGI WA THIONG’O, ROBERT OUKO, MARTIN SHIKUKU, MASINDE MULIRO, MOSETI ANYONA, FIELD MARSHALL MUTHOMI na FIELD MARSHALL DEDAN KIMATHI ambaye ardhi aliyopigania sasa inakaliwa na wakoloni weusi huku vizazi vyake vikiteseka.
- Mohammed Ali ni Mhariri Mkuu wa Kitengo cha Upekuzi KTN. Kuwasiliana naye: Twitter: @mohajichopevu